Pichani katibu Tawala Mkoa wa Mbeya Mariam Mtunguja wa tatu kulia aliye simama (Picha na Maktaba) |
Na EmanuelMadafa,Mbeya
SERIKALI Mkoani Mbeya imepiga marufuku itikadi za kisiasa katika uendeshaji
wa timu ya soka ya Mbeya City inayoshiriki Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara ili
kulinda uhai wa timu hiyo.
Uamuzi huo
umefikiwa kufuatia baadhi ya wanasiasa kuanza tabia ya kujinadi kuwa
mafanikio ya timu ya Mbeya City inayomilikiwa na Halmashauri ya Jiji la Mbeya
yametokana na juhudi zao na vyama vyao vya siasa.
Katibu
Tawala wa mkoa wa Mbeya, Mariam Mtunguja, aliyasema hayo kwenye hafla ya kuwapongeza
wachezaji, benchi la ufundi na viongozi wa timu ya Mbeya City iliyoambatana na
kuivunja rasmi kambi ya timu hiyo baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu ya Soka
Tanzania Bara huku timu hiyo ikifanikiwa kushika nafasi ya tatu.
Mtunguja, amesema
tayari baadhi ya wanasiasa mkoani hapa wameanza kuyahusisha mafanikio ya timu
hiyo na harakati zao za kisiasa za vyama vyao hali ambayo ni hatari kwa uhai wa
Mbeya City katika ulimwengu wa soka nchini.
Amesema,
tabia hiyo inaweza kuwagawa mashabiki wa timu hiyo kutokana na kwamba kila
mmoja ana mapenzi na chama chake cha siasa hivyo kuingiza itikadi kwenye
uendeshaji kutasababisha ubaguzi baina yao.
Kufuatia
mafanikio ya timu hiyo, Meya wa Jiji la Mbeya, Athanas Kapunga, amesema
Halmashauri ya jiji hilo imeamua kuboresha mishahara ya wachezaji ili kuzuia
uwezekano wa kurubuniwa na timu kubwa kwa kigezo cha maslahi.
Kwa upande
wake, Mwenyekiti wa Mbeya City, Musa Mapunda, amesema baada ya kufanikiwa
kushika nafasi ya tatu msimu huu, sasa wanaweka mikakati ya kuhakikisha timu
hiyo inachukua ubingwa wa ligi Kuu ya Soka Tanzania bara msimu ujao.
Naye kocha
Mkuu wa timu hiyo, Juma Mwambusi, alisema katika usajili wao kwa ajili ya msimu
ujao wa ligi hiyo hawatachukua wachezaji wenye majina kutoka timu zinazoshiriki
ligi hiyo bali bali ataangalia zaidi wachezaji chipukizi wasio na majina kutoka
ndani ya mkoa wa Mbeya.
Mbeya City
ilianzishwa Julai mwaka 2011 na huu ni msimu wake wa kwanza kushiriki ligi hiyo
na kupata mafanikio yak upigiwa mfano.
Mwisho
Post a Comment