Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa
Rais Muungano na Mazingira Mh. January Makamba akizungumza na Mtendaji
wa Kijiji cha Butu, Kata ya Jipe Wilayani Mwanga Bw. Nassor Abdul wakati
Waziri Makamba alipotembelea Ziwa Jipe ambalo limeathiriwa kwa kiasi
kikubwa na magugu maji ambayo yanasababisha kupungua kwa shughuli za
uvuvi ambazo ndio chanzo kikubwa cha mapato kwa wakazi wa eneo hilo.
Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Bw. Aron Mbogho.
Mifano kwa vitendo: Pichani
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mh. January
Makamba akiwa amembeba mtoto Meshack Ombeni katika Kijiji cha Butu
pembezoni mwa Ziwa Jipe. Waziri Makamba amewaasa wananchi hao kulinda
Ziwa hilo ili liweze kunifaisha vizazi vijavyo na kuwatahadharisha kuwa
uharibifu wa mazingira utahatarisha uhai wa ziwa hilo. .
Upungufu mkubwa maji katika bwawa
la nyumba ya Mungu. Inasemekana kupungua kwa kina cha maji kunatokana
na ukame wa muda mrefu na uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana na
shughuli za binadamu katika vyanzo vya maji vinavyopeleka maji katika
bwawa hilo ukiwemo Mto Kikuletwa.
………………………………………………………………………..
Na Lulu Mussa-Mwanga – Kilimanjaro
Imebainika kuwa Ziwa Jipe liko
hatarini kutoweka endapo hatua za haraka hazitachukuliwa katika
kulinusuru. Hayo yamesemwa leo na Waziri mwenye dhamana ya usimamizi wa
Mazingira Mh. January Makamba alipofanya ziara ya kukagua ziwa hilo
ambalo sehemu kubwa imezungukwa na magugu maji.
Waziri Makamba amesema kuwa ziwa
hilo ni rasilimali muhimu na hivyo ni lazima kuwe na mpango wa muda
mfupi na ule wa muda mrefu. Kupitia Baraza la Taifa la Hifadhi na
Usimamiza wa Mazingira (NEMC) ameazimia kutangaza kupita Tangazo la
Serikali kuwa eneo hilo ni eneo nyeti kimazingira.”Tutatanga eneo hili
kuwa eneo nyeti kimazingira na tutaweka masharti ya matumizi katika eneo
hili” Alisisitiza Makamba
Azimio hilo la kutangaza kuwa
eneo mahsusi ama nyeti kimazingira itasaidi katika kuandika maandiko
mbalimbali ya miradi na kupata fedha kutoka kwa wadau na washirika wa
maendeleo. Pia litawekwa chini ya uangalizi maalumu na kuweka masharti
ya matumizi bora ya eneo hilo. ” Tutaweka masharti makali na magumu
zaidi ili watakao kiuka wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria”
Aliongezea Waziri Makamba.
Aidha, Waziri Makamba amesisitiza
kuwa ni vema kunusuru ziwa hilo sasa maana ndani ya miongo 2-3 huenda
ziwa hilo likatoweka. “Bila hifadhi ya mazingira hakuna maisha, na
ukiyaharibu mazingira hakuna msamaha yatakuadhibu tu” Akiongea katika
Mkutano wa hadhara kijijini Butu, Waziri Makamba amesema kuwa shughuli
zozote za maendeleo iwe uvuvi, kilimo, utalii, mifugo kwa namna moja ama
nyingine zinategema hifadhi endelevu ya mazingira.
Katika hatua za muda mrefu Waziri
Makamba amewataka wasimamizi wa Bonde la Pangani, Wizaya ya Tawala za
Mikoa na Serikali za Mitaa, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Afrika Mashariki na Ofisi ya Makamu wa Rais kupitia Baraza la Taifa la
Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kukutana mara moja kuandaa
mpango na mtazamo wa pamoja wa kunusuru Ziwa Jipe.
Akiwa njiani kuelekea Nyumba ya
Mungu Waziri Makamba alipitia katika Kiwanda cha Kifaru Quarries Co. Ltd
na kukuta kikiendelea na uzalishaji wa kokoto bila kuwa na cheti cha
Tathmini ya Athari kwa Mazingira. Baraza la Taifa la Hifadhi na
Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeutaka uongozi wa Kiwanda hicho
kusitisha uzalishaji mara moja na kutakiwa kulipa faini kwa kukiuka
Sheria ya Mazingira kifungu namba 81 na 196.
Waziri Makamba pia amefanya ziara
katika Bwawa la Nyumba ya Mungu na kufanya mkutano wa hadhara na wakazi
wa kijiji cha Kakongo ambao kwa pamoja wamelalamikia zuio la kufanya
shughuli za uvuvi katika bwawa hilo kutokana na kupungua kwa kina cha
maji na samaki katika bwawa hilo.
Bw. Charles John Waziri Mkazi wa
Kijiji cha Kagongo amesema kuwa kuna hujuma katika matumizi ya
rasilimali maji ambapo imebainika kuwa wakulima wanaotumia kilimo cha
umwagiliaji wamekua wakitumia maji kwa kiasi kikubwa na kusababisha
upungufu katika bwawa.
Akijibu kero na malalamiko ya
wananchi hao Waziri Makamba ameagizia kufanyika kwa doria na kuainisha
pampu zote zinazovuta maji kutoka bwawani hapo “Naaagiza Mamlaka ya
Wilaya ya Mwanga, Serikali ya Mtaa na Mamlaka ya Bonde Pangani kufanya
doria na kuhakiki pampu zote kujua uhalali wake kama zimesajiliwa na
kama zinavibali, zitakazobainika kutokuwa na vibali zote zitaifishwe”
Alisisitiza Waziri Makamba.
Waziri Makamba yuko katika ziara
maalumu ya kukagua uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira, changamoto na
kuweka mikakati ya muda mfupi na muda mrefu wa kukabiliana nazo. Mpaka
sasa Waziri Makamba ameshatembelea Mkoa wa Pwani, Tanga na Kilimanjaro.
Post a Comment