Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Ndugu Abbas Kandoro
Na Mwandishi wetu,Mbeya
MKUU wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro, amesema kitendo cha Halmashauri ya Mbozi kupata hati yenye mashaka kwa miaka mitatu mfululizo hakivumiliki, hivyo anafikiria kuzishauri mamlaka zenye uwezo wa kufanya maamuzi hayo kuivunja Halmashauri hiyo ili kupata mfumo mpya wa kuiendesha.

Hatua hiyo imekuja baada ya ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa hesabu za serikali (CAG) kuonesha kuwa Halmashauri hiyo imepata hati yenye mashaka, huku  kiasi cha zaidi ya  shilingi bilioni 1 zilizopelekwa na serikali kwa ajili ya shughuli za maendeleo kukosa taarifa sahihi za kuhifadhi kumbukumbu za mahesabu.

Akizungumza katika kikao maalumu cha baraza la madiwani wa Halmashauri hiyo, kilichoketi juzi kwa ajenda moja tu ya kupitia mrejesho wa bajeti ya mwaka wa fedha 2013/14, Kandoro amesema kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ubadhirifu na wizi wa fedha za serikali katika Halmashauri ya Mbozi, anafikiria kuzishauri mamla zenye uwezo  kufanya maamuzi ya kuivunja Halmashauri hiyo ili kupata mfumo mpya wa kuiendesha.

Awali akitoa salamu za serikali baada ya kikao hicho kufunguliwa, Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Dk. Michael Kadeghe, alimuomba Mkuu wa Mkoa Kandoro kuchukua hatua dhidi ya watendaji  kwani vitendo vya ubadhirifu ndani ya Halmashauri hiyo vimekuwa ni vya mazoea.

Kutokana na ombi hilo, Kandoro alikiri kufanyika kwa vitendo hivyo na kwamba taarifa ya CAG, imeonyesha kuwa kwamba watendaji hao wamezigeuza fedha za serikali kuwa ni vitega uchumi vyao hivyo ni vema serikali ikachukua hatua za kisheria.

Amesema, ubadhirifu mkubwa  wa fedha umegundulika katika baadhi ya miradi ya maendeleo hususani kwenye  sekta za kilimo, afya, elimu na maji, ambapo kiasi cha zaidi ya shilingi bilioni 1 kutokuwa na taarifa wala kumbukumbu.

Ameyataja baadhi ya maeneo ya miradi ambapo fedha zimeonekana kutumika ndivyo sivyo au kuibwa kuwa ni shughuli za usafi na uhifadhi wa mazingira , kiasi cha shilingi milioni 408 zimeonekana kutumika bila maelezo ya kutosha.

Fedha nyingine kiasi cha shilingi milioni 106,889,500 zilitumika bila kuwepo na kumbukumbu za msingi kama vile vikao, majina ya wajumbe  hali ambayo iliashiria wazi kuwa kiasi hicho kiliibwa.

Aidha, Kandoro ameendelea kuainisha maeneo mengine kuwa ni Ujenzi wa maghara katika mji wa Mlowo kiasi cha shilingi milioni 70, ununuzi wa Pikipiki 92  kukosa stakabadhi za manunuzi.

Ameongeza kuwa, kiasi kingine cha fedha milioni 14 kilionekana kutumika kwa mashaka katika safari ya watendaji kwenda katika shughuli za nanenane, milioni 30 zilikosa kabisa maelezo miongoni mwa hoja za mkaguzi.

Kwa mujibu wa maelezo ya watendaji, gunia moja la mahindi hutozwa ushuru wa kiasi cha shilingi 2000 , hivyo katika gunia hizo 300 Halmashauri hiyo ilipaswa kupata kiasi cha shilingi 600,000.

Kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Mkoa Kandoro, amewataka madiwani kuwa makini katika kuwasimamia watendaji kwa kuwa wakali dhidi ya wezi na wabadhirifu  kwani huko ndiko kutetea maslahi wananchi waliowachagua.


Hata hivyo, alisikitishwa na taarifa kuwa kuna baadhi ya madiwani wanatuhumiwa kuwa ni sehemu ya mitandao ya wizi katika Halmashauri hiyo, kwani hilo linadhihirishwa pale fedha zilizotumwa katika kata zao zimetumika, lakini kazi hazionekani wala kufanana  na gharama.


mwisho

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala, Ushauri n.k.?Basi Wasiliana Nasi Simu/WhatsApp 0759 406 070

Post a Comment

 
Top