Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This

Watuhumiwa  wakifikishwa mahakamani 
Na EmanuelMadafa,Mbeya

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoani Mbeya, imewapandisha kizimbani watumishi wawili wa halmashuri  ya jiji la Mbeya, wakiwatuhumu kuomba hongo ya shilingi 150,000 kutoka kwa mwananchi Frank Mwakaluka.

Watumishi waliofikishwa mahakamani ni Alex  Anderson Kimaro na Julius Issakwisa Mwambulukutu ambapo mshitakiwa  namba moja  Alex Kimaro anakabiliwa na mashitaka mawili huku mshitakiwa namba mbili Julius Mwambulukutu akikabiliwa na shitaka moja.

Akiwasomea mashitaka hayo Mwendedsha Mashitaka wa Takukuru, Nimroad Mafwele, mbele ya hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama ya Wilaya  Girbelt Ndeuluo, alisema, watuhumiwa hao walitenda kosa hilo  November  26, 2013 katika eneo la Ilomba lililopo Jijini Mbeya ikiwa ni kinyume cha sheria namba 15(i)(a) ya kuzuia na kupambana na rushwa sura ya 11 ya mwaka 2007.

Amesema,  kwa nyakati tofauti watumishi hao wakiwa katika ukaguzi wa majengo walimkamata Franky Mwakaluka  kwa madai ya kushindwa kulipia jengo lake na kumuomba kiasi cha shilingi 150,000 ili wamuachie na kwamba  zoezi hilo lilifanyika ndani ya gari  ambalo ni mali ya halmashauri ya Jiji la Mbeya.

Aidha, Mwendesha mashitaka huyo, amemsomea shitaka la pili mshitakiwa namba moja ambaye ni Alex Kimaro.

Alisema mshitakiwa huyo akiwa katika ukaguzi wa majengo aliomba hongo ya shilingi 60,000 kwa Green Mwakionya ili amuachie huru Franky Mwakaluka waliyekuwa wamemkamata kwa madai ya kutolipia kodi ya pango.


Baada ya watuhumiwa hao kusomewa makosa mbalimbali, mwanasheria huyo alisema dhamana ipo wazi na masharti ya dhamana lazima yazingatiwe kwa mujibu wa vifungu vya sheria vya kosa vinavyoeleza.

Hata hivyo, baada ya mwanasheria huyo kuwasilisha maombi hayo, hakimu Ndeuruo, alisema  dhamana ipo wazi kwa washitakiwa wote wawili na kwamba kila mshitakiwa atatakiwa kudhaminiwa na mtu mmoja  kwa kiasi cha shilingi milioni moja na kwamba kesi hiyo itasikilizwa tena Oktoba 13 mwaka huu.


Washitakiwa wote walikana mashitaka  na kwamba wapo nje kwa dhamana baada ya kufanikiwa kudhaminiwa.

Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala, Ushauri n.k.?Basi Wasiliana Nasi Simu/WhatsApp 0759 406 070

Post a Comment

 
Top