| Baadhi ya Wakuu wa Wilaya Mkoani Mbeya wakiwa makini kumsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Mbeya katika kikao hicho. |
Na EmanuelMadafa
SHIRIKA la Ugavi wa Umeme Tanesco, limeweza kusambaza umeme kwa watu 407,400 sawa na asilimia 15.5 ya wakazi wa Mkoa wa Mbeya.
Akielezea mafanikio ya utekelezaji wa mpango wa matokea makubwa sasa(Big Results Now) kwa mwaka wa 2013/2014, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro alisema licha ya jitihada hizo lakini bado kuna mahitaji makubwa ya umeme katika maeneo ya mijini na vijijini hususani katika viwanda na taasisi za umma.
Amesema, Mahitaji ya umeme katika Mkoa wa Mbeya yamefika megawati 38 na watumiaji wa umeme walioko ni 70,000 kati ya 2,100 ni wa Taasisi za umma, viwanda na biashara huku wateja 67, 900 ni kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.
Amesema, Mtandao wa umeme umefika katika kila Makao makuu ya Wilaya na baadhi ya maeneo vijijini isipokuwa Wilaya mpya ya Momba ambapo taratibu za kumpata mkandarasi wa kusambaza umeme zinaendelea licha ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali.
Amesema, chini ya wakala wa Uendeshaji nishati ya Umeme Vijijini (REA) awamu ya pili, umeme utasambazwa katika vijiji 170 na kwamba zabuni ya ujenzi wa miundombinu ya kupeleka umeme imetangazwa na wakanadarasi wawili wamepatikana.
Amesema, idadi ya vijiji vitakavyounganishiwa umeme kiwilaya ni Kyela vijiji vitatu, Mbozi vijiji 28, Halmashauri ya Mbeya vijiji 29, Rungwe vijiji 45, Mbarali vijiji 37, Chunya vijiji 20, Momba kijiji kimoja na Ileje vijiji 19.
Hata hivyo, amesema kuwa miradi hiyo itagharimu shilingi Bilioni 82.86 na inatarajiwa kuwaunganishia umeme wateja 11,160 mradi wa REA awamu ya pili na kukamilika kwake ni mwaka 2015.







Post a Comment