Na EmanuelMadafa,Mbeya
KATIBU Mkuu Ikulu, Peter
Ilomo, amewataka watendaji wa Sekratieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma
kuzingatia maadili ya kazi yao kwa kutunza siri za sekretarieti hiyo kuhusu
taarifa mbalimbali za viongozi wanaoshughulikiwa na chombo hicho.
Ilomo, alitoa changamoto
hiyo, wakati akifungua Mkutano wa 12 wa Baraza la Wafanyakazi wa Sekretarieti
ya Maadili ya viongozi wa Umma unaofanyika kwa siku mbili Jijini Mbeya.
Amesema, changamoto kubwa inayoikabili sekretarieti hiyo ni namna ya utunzaji wa siri za viongozi mbalimbali
wanaochunguzwa na mamlaka hiyo katika utendaji kazi wake wa kawaida hivyo wakati umefika kwa watendaji kuhakikisha wanazingatia maadili yao ili kukifanya chombo hicho kuaminika kwa wananchi.
Ilomo amesema
Sekretarieti hiyo inautaratibu wa kukusanya na kutoa taarifa za viongozi
wanaofanyiwa kazi hivyo watendaji hao wanapaswa kuzingatia utaratibu huo ambao
ni sehemu ya maadili yao.
Awali akimkaribisha
Ilomo kufungua mkutano huo, Kamishna wa Maadili wa Sekretarieti ya Maadili ya
Viongozi wa Umma, Salome Kaganda, amesema licha ya majukumu makubwa ya
sekretarieti hiyo lakini bado inakabiliwa na upungufu wa watumishi na hivyo
kuiweka katika wakati mgumu kiutendaji.
Kaganda, amesema hadi sasa Tanzania ina viongozi 13,167 wanaofuatiliwa na sekretarieti hiyo lakini mamlaka hiyo ina watumishi 200 hivyo kukosekana kwa uwiano mzuri kiutendaji.
Pia Kaganda, amesema bado suala la mgongano wa kimaslahi ni changamoto nyingine kwa sekretarieti hiyo kutokana na baadhi ya viongozi kumiliki biashara zinazopaswa kukaguliwa huku wenyewe wakiwa hawapo tayari kusema ukweli kuhusu umiliki wa mali hizo.
Mkutano huo wa siku
mbili unawahusisha viongozi wa sekretarieti hiyo kutoka kanda ya
Kaskazini inayohusisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro na Manyara, Kanda ya Ziwa
inayoundwa na mikoa ya Mwanza, Geita, Mara na Kagera, Kanda ya Magharibi yenye
mikoa ya Tabora, Kigoma, Simiyu na Shinyanga, Kanda ya ya Kati mikoa ya Dodoma
na Singida, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya,
Katavi na Rukwa, kanda ya Kusini mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma huku
Kanda ya Mashariki ikiwa na mikoa ya Tanga, Morogoro na Pwani.
Mwisho










Post a Comment