Share this PostPin ThisShare on TumblrShare on Google PlusEmail This
      Askofu  Mkuu Kanisa la Moravian Jimbo la Kusini Magharibi 
KANISA LA MORAVIAN TANZANIA,
JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI,
USHIRIKA WA BETHLEHEMU,
S.L.P. 905,
MBEYA

28/06/2014


ASKOFU ALINIKISA CHEYO,
JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI,
S.L.P 377,
MBEYA.


YAH: KUJIUZURU NAFASI YA UASKOFU ASKOFU ALINIKISA CHEYO

Tafadhali rejea  kichwa cha habari hapo juu chahusika.

Baraza la Wazee Kanisa la Moravian Ushirika wa Bethlehemu lililofanyika tarehe 28/06/2014 katika ajenda zake mojawapo walijadili kuhusu mgogoro unaoendelea katika Jimbo la Kusini Magharibi. Wajumbe walijadili kwa kina kuhusu mgogoro huo na kupitia mambo mengi hivyo waliamua kuwa ili kulinusuru Kanisa kuendelea kuwa na migogoro isiyo ya lazima linatoa tamko kuwa Askofu Alinikisa Cheyo ajiuzuru mora moja ili kuleta amani ndani ya Jimbo letu.

Mchanganuo kuhusu mgogoro huo umeambatanishwa.

Tunakutakia utelekezaji mwema,




………………………………………………                         …………………………………………
         MWANDISHI                                      M/KITI WA BARAZA LA WAZEE       
           USHIRIKA                                       USHIRIKA WA BETHLEHEMU

Nakala
1.            Mkuu wa Wilaya
2.            Mkuu wa Wilaya wa polisi (OCD)
3.            Wakuu wa Idara na Taasisi za Kanisa
4.            Shirika zote za Jimbo




TAARIFA YA UCHAMBUZI WA MGOGORO WA HALMASHAURI KUU YA JIMBO, JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI (JKM) DHIDI YA MWENYEKITI MCH. NOSIGWE BUYA NA UHUSIKA WA ASKOFU ALINIKISA CHEYO

Ndugu zangu wapendwa, mgogoro huu umeleta madhara makubwa katika Kanisa, na kuligawa Kanisa letu katika vipande vipande ambalo katika historia yake. Mgogoro huu umesababisha kutoelewana kati ya uongozi wa Jimbo wao kwa wao, Halmashauri kuu ya Jimbo, kamati tendaji na kuleta migongano kati ya Kamati tendaji na Shirika, wachungaji kujigawa katika makundi. Hivyo mgogoro huu umeleta uhasama kati ya mchungaji na mchungaji, ushirika na ushirika, mchungaji na wakristo wake, uhasama usiokoma. Wachungaji kutoelewana na uongozi wa Wilaya, Mtaa n.k. Hili jambo ni kubwa ingawa wengine wanatofautiana kimtazamo, viongozi wa juu wa Kanisa, Wachungaji na Wakristo kwa ujumla.  Lakini ukweli kuwa jambo hili ni kubwa na lina madhara makubwa kwa Kanisa na endapo halitapatiwa ufumbuzi litazidi kuleta madhara makubwa zaidi. Uchambuzi wetu kuhusu jambo hili tumeona kuwa linamhusu sana Askofu Alinikisa Cheyo kuwa mhusika mkuu wa chanzo cha tatizo la mgogoro huu kwa kukiuka Katiba ya Kanisa letu mara kadha, kiasi kwamba amebadilisha nafasi yake ya Uaskofu na kuwa mtendaji mkuu badala ya kulisimamia Kanisa kwa ushauri na usuluhishi.  Yeye ameingia kiutendaji zaidi na dhamiri ya kumuondoa Mwenyekiti Mch. N. Buya huku akijua kabisa kuwa anafanya makosa ya kikatiba kwa kufanya mapinduzi, rejea Katiba ya KANISA LA MORAVIAN TANZANIA JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI IBARA YA 33, KUFUNGU B, Kipengele cha namba tatu ya kirumi (III) wajibu wa Askofu “………….wote wanaweza kumwendea kwa shida zao za kiroho moja kwa moja, yeye huwashauri, huwaonya, huwafariji na kuwaongoza kiroho bila kukata mambo yeyote kisheria na kuyapeleka kwenye Halmashauri kuu ya Jimbo” 

Pia  alichukuwa nafasi ya maamuzi ambayo yeye kikatiba siyo Mwenyekiti, hapa pia  alikiuka Katiba, Ibara ya 33, Kifungu B, kipengele cha namba nane ya kirumi (viii)  “Rejea Katiba “………….Anaweza kukaribishwa katika vikao vya kamati tendaji.”

Hivyo uchambuzi upo kama ifuatavyo:-

(a)  Mwanzo wa chimbuko la mgogoro ilitokea mnamo tarehe 30/04/2013 ambapo Halmashauri kuu jimbo ilikutana Agenda ilikuwa kujadili utendaji mbovu wa kamati tendaji. Na katika kikao hicho walimtaka Mwenyekiti atoe taarifa ya Tshs 200,000,000/= (millioni mia mbili) za Sekondari za ujenzi wa shule. Na vilevile Makamu Mwenyekiti Z. Sichome alikuwa ameagizwa alete taarifa ya maandishi ya jinsi anavyotimiza wajibu wake kikatiba, kusimamia majengo, kufuatilia mkopo wa ujenzi wa Tshs Millioni mia mbili(200,000,000/=) , taarifa yake ikakataliwa maana haikuonyesha jinsi alivyotimiza wajibu wake, rejea IBARA 35, KIFUNGU CHA 2wajibu wa Makamu Mwenyekiti kipengele F. “ Kuangalia kazi zote za majengo katika Jimbo akishirikiana na Mwenyekiti wa Wilaya ambapo majengo yapo na kutoa taarifa kwa Kamati tendaji kwa utekelezaji”. Kikao kiliona kina uwezo wa kuamua maamuzi magumu bila kuvunja amani, hivyo Askofu aliamrisha Kamati tendaji watoke nje ya kikao  (Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na katibu) kisha kikao kilikwenda mbali zaidi kikamtoa mtunza hazina na mkaguzi wa ndani nje ya kikao. Hivyo safu yote ya uongozi huo ikawa nje ya kikao. Baada ya hapo akachaguliwa Ndugu Hakimu Mwandenuka kuwa Mwenyekiti wa kikao cha Halmashauri kuu ya Jimbo kwa uamuzi huo ulikiuka Katiba Ibara 10: 2C rejea “Kamati tendaji” Mwenyekiti  na Makamu wawe wachungaji”  Imekuwaje Mkristo asiye Mchungaji achaguliwe kushika nafasi ya Mwenyekiti wa Jimbo? Na kwa nini Askofu A. Cheyo akubali kukiuka katiba kiasi hicho?. Hapa inaonyesha kuwa Askofu ndiye chanzo cha tatizo la mgogoro.

(b) Baada ya mazungumzo ya kikao,  kamati tendaji na walotolewa nje waliitwa kuingia kwenye kikao. Maamuzi yalikuwa:-

(i)           Makamu Mwenyekiti Mch. Z. Sichome afuatilie kwa makini kazi ya ujenzi na usimamizi wa majengo na atimize majukumu yake kikatiba (Ibara ya 35:2F).
(ii)          Mwenyekiti Mch. N. Buya asimamie vema majukumu yake, na maamuzi ya Halmashauri kuu ya Jimbo ilimwagiza awapeleke Mahakamani Ndugu Ambakisye Kabango na Dada Grace A. Mwalukuta kabla ya kikao cha tarehe 31/07/2013 vinginevyo maamuzi magumu yatachuliwa dhidi yake.

KUSIMAMISHWA MWENYEKITI N. BUYA

Kikao  cha Halmashauri kuu ya Jimbo kilikutana tena tarehe 30/07/2013 kikiongozwa na Mwenyekiti N. Buya. Baadae katika mazungumzo Askofu Alinikisa Cheyo aliwaamuru Kamati tendaji (Mwenyekiti, Makamu na Katibu), Mtunza hazina na Mkaguzi wa ndani watoke nje ya kikao. Baada ya kutolewa wajumbe hao ndugu Charles Mwakipesile alichaguliwa kuwa Mwenyekiti na Mch. Stephano Mbalwa kuwa mwandishi. Jambo la kushangaza kwa makusudi kabisa Askofu alirudia kufanya jambo lile lile la ukiukaji wa Katiba.  Uamuzi ukatolewa wa kumsimamisha Mch. N. Buya kwa nafasi ya Mwenyekiti kwa sababu hajampeleka Ndugu A. Kabango na G. Mwalukuta mahakamani kwa matumizi mabaya yaTshs 200,000,000/=, ambapo kikatiba mwenye kazi ya kutoa taarifa za Vyuo na Shule za Sekondari Mbozi ni katibu alipaswa awajibike. Rejea Katiba Ibara ya 36, kipengele cha namba sita ya kirumi (vi) kinasema “kupokea na kuzingalia taarifa za kazi za makatibu wa idara za umoja wa wanawake ………….elimu ya kikristo, shule ya sekondari Mbozi na chuo cha ufundi”

Rejea barua Kumb. Na KMT. JKM 2 ya tarehe 31/07/2013 yenye kichwa cha habari kisemacho YAH: KUSIMAMISHA MCH. N. BUYA UONGOZI iliyowekwa saini na Ndg. Charles Mwakipesile ambayo haikuwa na muhuri wa Ofisi ya Jimbo, ikimtaka Mwenyekiti akabidhi Ofisi kwa Makamu Mwenyekiti.   Hapa tunahoji Ndg. C. Mwakipesile  alimwandikia Mwenyekiti N. Buya barua akiwa kama nani na kwa Katiba gani?

Kwa ujumla unaweza kuona Askofu A. Cheyo jinsi alivyoendelea kulitumbukiza Kanisa kwenye mgogoro mkubwa inakuwaje maamuzi ya kumsimasisha M/Kiti wa Jimbo aliyechaguliwa na Sinodi asimamishwe na kuandikiwa barua na mjumbe wa wakristo? Je Askofu analiona hilo kuwa ni jambo dogo? Askofu A. Cheyo anajihesabu anatoa ushauri, anatoa ushauri gani kwa Kanisa kuona mambo yanaenda hivyo kama katiba inavyomtaka katika Ibara ya 33 kifungu cha wajibu wa Askofu, kipengele  cha iii, “……yeye hushauri, huwaonya, huwafariji na kuwaongoza kiroho bila kukata mambo yoyote kisheria wala kuyapeleka kwenye Halmashauri kuu ya Jimbo” Tuonavyo sisi Askofu Cheyo amepania kuligawa Kanisa, ametoka kabisa kwenye wajibu wake, Ibara ya 33 …Askofu ni “ mhudumu wa Kanisa la umoja wa ndugu (Unitas Fratrum) akikaa katika Jimbo lake na kuongozwa na Katiba ya Jimbo chini ya Kanisa la umoja wa ndugu” kama ni hivyo mbona sasa haongozwi na Katiba na anakiuka Katiba ambayo yupo chini yake

TAARIFA YA TUME ILIYOUNDWA NA HALMASHAURI KUU YA JIMBO     KUCHUNGUZA TUHUMA ZA MWENYEKITI MCH. N. BUYA.

Mnamo  tarehe 20/11/2013 Halmashauri kuu katika kikao chake ilipokea taarifa ya Tume, iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Tume Ndugu Hakimu Mwandenuka.    Taarifa ya Tume ilibeba mambo  makuu mawili kama ilivyokuwa imeelekezwa na Halmashauri kuu ya Jimbo kuyachunguza juu Mwenyekiti  Mch. N. Buya ilikuwa kama ifuatavyo:-

a)    Tuhuma kuwa Mchungaji Noswigwe Buya kushindwa kusimamia masuala ya fedha.

b)   Kutosimamia maamuzi ya Halmashauri kuu ya Jimbo

Tume baada ya uchunguzi  ilibaini kuwa Mwenyekiti Mch. N. Buya hahusiki katika ubadhilifu wowote na wala hakuna  ushahidi wowote ulioonyeshwa  yeye  kuhusika, isipokuwa Tume  iliwatuhumu Makamu M/Kiti na Katibu Mkuu kuwa hawakuweza kusimamia na kumsaidia Mwenyekiti  alipokuwa hayupo.  Hivyo  kulikuwepo uzembe wakati wa uongozi wake.  Rejea Taarifa ya Tume Ukurasa wa 23 (nukuu),
1.     Tume ibaini kuwa katika tuhuma mbili zilizoelekezwa kwa Mwenyekiti Mch. N Buya zilizohusiana na mkopo wa Tshs. 200,000,000/- na kushindwa kusimamia suala zima la fedha, imebaini kuwa Mwenyekiti hakuhusika wala hakuna ushahidi wowote wa kufuja fedha hizo bali imebaini kuwa kulikuwa na uzembe katika uongozi wake kusimamia hayo.
2.     Tume imebaini kuwa Makamu Mwenyekiti Mch. Z. Sichone na Katibu Mkuu Mch. W. Mwansile hawakutimiza wajibu kikatiba wa kumsaidia Mwenyekiti katika masuala hayo hasa pale Mwenyekiti alipokuwa hayupo.

Taarifa hiyo Askofu aliikataa na kuelekeza  shutuma zake moja kwa moja kwa Tume kuwa Tume imembeba Mch. N. Buya, jambo hilo lilizua mgawanyiko  katika Halmashauri kuu ya Jimbo. Wajumbe wakataka kura ipigwe ya kumrudisha au kumwondoa katika wadhifa wake, Askofu alikataa akasema; kura haitatupa majibu  sahihi.  Hivyo kura haikupigwa.  Kikao  hicho kiliahirishwa  mpaka tarehe 20/12/2013.  Wakati wajumbe kikao hicho Askofu  alianza kukutana na wajumbe wachache wachache  wa Halmashauri  kuu ya Jimbo ili kuwashawishi wasimrudishe Mch. N. Buya. Kikao kilifanyika tarehe 30/12/2013.

Katika uchunguzi wetu tumeona jinsi Askofu alivyo kwenye mstari wa mbele kuigawa Halmashauri kuu ya Jimbo na kuendelea kushirikilia msimamo wake wa kutomtaka Mch. N. Buya kurudi kwenye wadhifa wake. Na ametumia njia ya kuwagawa Halmashauri ili kwake iwe rahisi kuitawala na ni kinyume cha Katiba.  Askofu hatakiwi kuingilia utawala na kuwa  mtawala bali awe mpatanishi, tunajiuliza katika hili  je amefanya upatanishi gani?

KUONDOLEWA UONGOZI M/KITI MCH. NOSIGWE BUYA

Mnamo tarehe 30/12/2013  kikao  cha Halmashauri kuu ya Jimbo kilikutana, katika kikao kile kilifikia hatua ya kumwondoa Mch. N. Buya kwenye uongozi  wa kuwa Mwenyekiti, kinyume na Katiba.  Katika Katiba  hakuna kifungu kinachoruhusu  Halmashauri kuu kumwondolea dhamana  ya Mwenyekiti uongozi bali kama Board itaona  anatuhuma za kimaadili au vitendo vinavyoonyesha kujitenga  kwake.  Katiba  inatoa maelekezo kuitishwa kwa Sinodi ya pekee kwa uamuzi rejea Katiba ya Ibara ya 9, kifungu cha 3 kipengele cha (iii)  “Sinodi ya pekee yaweza kuitishwa wakati wowote na Halmashauri kuu ya Jimbo  (PB) kwa kutoa taarifa ya miezi isiyopungua miwili. Sinodi hii itashauriana tu katika jambo ambalo kwalo imeitwa “ lakini katika kikao kile askofu A. Cheyo aliamuru kura ipigwe ili kumwondoa Mwenyekiti, tunajiuliza je Askofu  kufanya haya haoni alikiuka  Katiba?.   Ikumbukwe  kuwa kikao cha tarehe 20/11/2013 wajumbe walipendekeza kura ipigwe, lakini Askofu  alikataa, baada ya kuona wajumbe  wengi wameikubali taarifa ya Tume lakini baada ya  ushawishi wake kwa baadhi ya wajumbe, kikao cha tarehe  30/12/2013 akawashawishi wajumbe wapige kura.

Ukiangalia muda tulipofanya Sinodi ya uchaguzi  ya Mwaka 2012 na mwezi wa nne 2013 si muda mrefu  kwa hiyo tathimini ya kazi yake kwa Mch. N. Buya alianza tangu nyuma. Kama ni hivyo kwanini asitoe hoja yake mbele ya Sinodi kuwa hana imani na Mch. N. Buya mpaka akasubiri achaguliwe na ndipo aanze mizengwe?. Hapa inaonyesha wazi jinsi Askofu anaonekana wazi jinsi anavyotumia vibaya wadhifa wake wa Uaskofu kulivuruga Kanisa. 

Jambo la kushangaza katika barua  iliyoandikwa  na Mch. Zakaria Sichone Makamu mwenyekiti ya kuondolewa wadhifa wa kuwa Mwenyekiti Mch. N. Buya.  Mch. Sichone anataja kuwa Mch. N. Buya ameondolewa kwa makosa 11  (kumi na moja)  bila ya kuyataja  kurejea yale mawili yaliyochunguzwa  na Tume, je haya makosa 11 (kumi na moja) yametoka kwenye Tume ipi? na iliyoundwa na nani? Badala ya ile ya kwanza iliyoongozwa na Ndg. Hakimu Mwandenuka? Je, Askofu ameziona njama hizo au hazioni na kama ameziona ameyashughulikia kwa kiwango gani? Tunadiriki kusema yeye anajua na amekubali uchafu huo ufanyike ili kulichafua Kanisa

JITIHADA ZA KUTAFUTA SULUHU LA KUTATUA MGOGORO

a)    Tarehe 18/01/2014 Mch. N. Buya Mwenyekiti aliitisha Sinodi katika Ushirika wa Bethlehemu (barua ya tarehe 2/01/2014) aliomba iitishwe Sinodi ili  kutoa maelezo  kwa maamuzi  ya Halmashauri  ya kumsimamisha.

-      Lengo lilikuwa Sinodi iliangalie jambo hili ili suluhisho  lipatikane, kama Katiba  inavyosema.   Ushirika wa Bethlehemu ulipokea ombi hilo na kuwa tayari  kuchangia chakula.  Kwa kipindi hicho jitihada mbalimbali ziliendelea na watu mbalimbali kuishauri Kamati tendaji na Halmashauri kuu kuliangalia jambo hilo  lisilete mgawanyiko. Hivyo  Sinodi ilitangazwa kwa njia ya Barua,  Redio Baraka FM na Mch. N. Buya.

Askofu  Alinikisa Cheyo aliingilia kati baada ya kupata taarifa kuwa Sinodi imeitishwa, alimwagiza Mch. Z. Sichone akasitishe tangazo Redio Baraka FM  lisiendelee kutangazwa  na aliporudi  kutoka ziara yake Iringa, alikwenda  yeye na Makamu na Katibu walipinga na kutangaza kuwa Sinodi siyo halali,  Askofu akiwa mstali wa mbele  kiutendaji.  Katika hili linatupa picha halisi inaonyesha jinsi alivyohama kwenye huduma ya Uaskofu na kujiingiza kwenye kamati ya utendaji kwa kufanya hivyo amekuwa kinara wa mgogoro.

b)   Usuluhishi  wa Mch. Angolwisye Malambugi (M/Kiti Mstaafu) juu ya jambo hili  liliendelea kuvuta kasi ya mgogoro akiingilia kati na kuwakutanisha kamati tendaji na Mch. Nosigwe Buya ili walitengeneze jambo hilo, katika mazungumzo  hayo walifikia muafaka  kuwa M/Kiti Mch. N. Buya arudi kwenye nafasi yake na Jambo  hilo liende Halmashauri  kuu ya Jimbo  kupata baraka ya ridhaa yao. Na kumsisitiza  Mch.  N. Buya aandike barua ya kusitisha  Sinodi  iliyoitishwa  na wakapatana kwenda Baraka FM  kutoa sitisho  hilo kwa lengo  la patano hilo.  Pamoja na jitihada zote hizo kikao cha Halmashauri  kilipokutana na Askofu A. Cheyo  aliporudi  toka Kenya. maamuzi  katika Halmashauri hiyo yalikuwa ya peke yao hawakuwa tayari kukutana na Malambugi msululishi wa mgogoro huo bali uamuzi wao ulikuwa kinyume na patano na kuamua:-

(i)           Mch. N. Buya asirudishwe kwenye nafasi yake
(ii)          Mch. N. Buya apangiwe kituo kingine cha kazi aende Elimu ya kikristo akufundishe shuleni
(iii)        Ahame kwenye nyumba anayoishi aende sabasaba nyumba anapokaa Chimwemwe Mkurugenzi wa Radio Baraka F.M/

Tarehe 29/01/2014 Makamu mwenyekiti Mch. Z. Sichome alimwandikia  barua Mch. N. Buya ya kumtaka ifikapo tarehe 07/02/2014 awe amehama kwenye nyumba anaiyoishi.


c)    Katika kutaka kutatua mgogoro huo, kundi la wachungaji lilijitokeza kwa kujaribu njia mbalimbali wengine kwa kuandika barua kupeleka Jimboni, wengine kwa meseji za simu n.k. pamoja na yote hayo wachungaji wapatao 25 waliandika pingamizi lao kuhusu maamuzi yaliyochukuliwa na Halmashauri kuu :-
(i)           Kusimamishwa Uenyekiti wa Jimbo Mch. N. Buya
(ii)          Kupangiwa kituo kipya cha kazi maana Sinodi ilikwisha mpangia kituo hivyo hawezi kuondolewa bila ridhaa ya Sinodi
(iii)        Kupinga uhamisho aliopangiwa Mch. N. Buya.

d)    Wakristo na Mabaraza ya wazee nao walijitokeza kwa nyakati tofauti kujaribu kuwaona Kamati tendaji kuomba waitishe Sinodi ili kutatua mgogoro huo. Yote haya yaligonga ukuta, Askofu A. Cheyo alikataa kuitisha Sinodi na kuona kuwa hakuna tatizo lolote na kusema Wachungaji hao hawajui Katiba.  Hayo aliyasema kwa nyakati tofauti akiwa Kenya kwa njia ya mtandao wa Redio bomba FM na katika vikao alisema hawezi kuitisha Sinodi pia Shirikani aliendeleza sentesi hizo.

Tunajiuliza hivi kweli huyu Askofu analitakia mema Kanisa hili? Anakataa njia za mazungumzo, anakatakaa upatanishi, anatakataa Sinodi ambayo ndicho chombo cha mwisho cha kutatua matatizo ya Kanisa, Je Askofu amepotea kiasi gani? Haya yote anafanya kwa makusudi, kwa nini anahofu Sinodi?

  
USULUHISHI WA MH: MKUU WA WILAYA NA MKUU WA POLIISI (OCD)  Mkuu wa Wilaya (W) ya Mbeya Mheshimiwa Dr.  Normam Sigalla aliitisha kikao na wajumbe wa Kamati tendaji, Askofu Cheyo, Mch. N.Buya na uwakilishi wa wachungaji mmoja ambaye ni Mch. Mwiligumo, wawakilishi wa wakristo Ndg F. Phiri na Joseph Kajinga, OCD na Mkuu wa Upelelezi (DCI), katika mazungumzo ya upatanishi muafaka ukakubalika kwa pamoja kuwa kamati tendaji ikaitishe Halmashauri kuu ya jimbo ili iitishe Sinodi.  Askofu Alinikisa Cheyo mbele ya Halmashauri kuu alikataa kuitisha Sinodi na kuwaambia wajumbe kuwa Mkuu wa Wilaya alikuwa anawaburuza tu. Kwa mara ya pili tena Mkuu wa Wilaya ya Mbeya alikutana na kamati tendaji, katika mazungumzo hayo muafaka ukawa jibu sahihi ni Sinodi na mapatano yakawa  baada ya Pasaka mwezi wa nne kuanzia tarehe 1/05/2014 mpaka tarehe 30/06/2014 muwe mmeitisha Sinodi Askofu hakuwepo. Tarehe 13/05/2014 walipoita Bodi, bado Askofu alisikika akisema Sinodi haitaitwa mpaka Sinodi ya mwaka 2016. Mkuu wa Wilaya hawezi kutuamulia mambo yetu, wakati huo huo anaenda Shirikani kufanya uchochezi kwa kumtangaza Mch. B. Buya kuwa ni mwizi na kumchafua zaidi  kwa mfano:-


-      Alikwenda Ushirika wa Ruanda mbele ya Ibada na kusema Mch. N. Buya amekula Tshs 600,800,000/= (millioni mita sita la laki nane) na kuwauliza wakristo Je tumrudishe tena Mch. N. Buya mbadhilifu na ninyi ni watoaji wazuri?, hatuwezi kumrudisha Buya. Hii inaonyesha ni uchochezi wa hali ya juu.

-      Pia alikwenda Makongolosi Chunya nako amesema hayo hayo, kaenda Mtaa wa Songwe alikuwa anaanza kusema hivyo hivyo na alipomuona Mch. N.  Buya anaingia Kanisani akabadilisha usemi, kuwa sisemi Mch. N. Buya amekula hizo pesa

.
Hivyo baada ya mchanganuo huu Ushirika wa Bethlehemu tunatoa tamko lifuatalo

-      Askofu Alinikisa Cheyo ajiuzuru wadhifa wake wa Uaskofu mara moja kwa kukiuka na kuilinda Katiba ya Kanisa la MORAVIAN TANZANIA JIMBO LA KUSINI MAGHARIBI Ibara ya 33:i pia kukiuka wajibu wake kama Askofu kama inavyoelekezwa IBARA 33, Kifungu cha B, Kipengele i, ii, iii, na iv kwa kuacha huduma ya Kiaskofu na kujitwalia madaraka ya kiutendaji na kuendelea kufanya uchochezi kwenye Shirika mbalimbali anazotembelea.

TAMKO HILI LIMETAMKWA NA BARAZA LA WAZEE USHIRIKA WA BETHLEHEMU





………………………………………………                              …………………………………………
MWANDISHI WA BARAZA                          MWENYEKITI WA BARAZA
LA WAZEE - BETHLEHEMU                         LA WAZEEE, USHIRIKA WA
                                                                             BETHLEHEMU      


Je, Una Habari,Picha,Tangazo,Makala, Ushauri n.k.?Basi Wasiliana Nasi Simu/WhatsApp 0759 406 070

Post a Comment

 
Top